
Kwa ufupi
Katika mafundisho ya kanisa hilo, wanandoa hawaruhusiwi kutengana hadi kifo, labda iwe kwa sababu chache, zikiwamo zinaa.
Vatican City, Vatican. Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis anafikiria kufanya mabadiliko makubwa katika kanuni za ndoa zinazozuia wanandoa kutengana bila kibali cha kanisa hilo.
Katika mafundisho ya kanisa hilo, wanandoa hawaruhusiwi kutengana hadi kifo, labda iwe kwa sababu chache, zikiwamo zinaa.
Hata hivyo, juzi Papa Francis alieleza uamuzi huo unatokana na ugumu mwingi ambao wanandoa wanaofikiria kutengana wanaupata kwa sasa.
Kwa sasa, waumini wa Kikatoliki wanakumbana na vikwazo vingi katika kutengua ndoa zao kisheria.
Kikanuni, ndoa ni sakramenti ndani ya kanisa hilo ambayo ikishafungwa basi haifunguliwi.
Papa Francis alieleza ugumu huo umewafanya baadhi ya maofisa wa kanisa hilo kujinufaisha kwa ada zinazofikia maelfu ya dola, wanazotoza kama gharama za kusimamia kesi zinazohusu kutenguliwa kwa ndoa.
Aliwaambia maofisa wa kanisa hilo wanaoshughulikia utenguaji wa ndoa hizo wanaohudhuria semina maalum mjini Vatican kwamba akiwa askofu wa Buenos Aires, Argentina aliwahi kumtimua kazi ofisa aliyedai dola ili kushughulikia suala la kutengua ndoa.
Alieleza kuwa wakati ule alishangaa kuona baadhi ya waumini wakipata shida kushughulikia ndoa zao, wakisafiri umbali mrefu, kupoteza muda kwenda kwenye mahakama za kanisa.
Alifichua jinsi alivyomtimua kazi ofisa aliyedai dola 10,000 kushughulikia suala hilo.
“Lazima tuwe makini, mchakato huu usigeuzwe kuwa biashara kwa wengine,”alieleza Papa Francis.
Uamuzi huo ni mtihani kwenye mafundisho ya kanisa hilo kuhusu ndoa ambayo ni sakramenti inayoheshimika, isiyoruhusiwa kufunguliwa kwa njia ya talaka.
Waumini wengi wa Kikatoliki ambao wamekuwa wakitaka ndoa zao zitenguliwe, hulazimika kuomba kibali, kanuni ya kanisa ambayo lazima ibatilishe kwanza muungano wao, kwamba ulikuwa wa lazima au haukuwapo.
0 comments:
Post a Comment