Pamoja na kuwepo kwa changamoto za kushuka kwa bei ya mafuta duniani, Tanzania bado imeendelea kuvutia wawekezaji kutoka pande zote za Dunia kuja kuwekeza katika shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi nchini.
Akiongea katika mkutano wa mwaka wa GE Oil & Gas, Waziri wa Nishati na Madini Mhe. George Simbachawene (MB) aliwaalika wawekezaji wakubwa kutoka pande zote za dunia kutembelea Tanzania na kuona nafasi za uwekezaji zilizopo.
Mkutano huo uliofanyika Florence, Italy uliwakutanisha wadau wakubwa wa Mafuta na Gesi duniani kujadili changamoto katika sekta hiyo na namna ya kuzikabili. Kauli mbiu ya mwaka huu ililienga zaidi kuangalia namna ambavyo sekta hii itachochea maendeleo ya dunia nzima kwa kuhakikisha kuwapo kwa nishati endelevu na yenye kujali mazingira.
Tanzania iliwakilishwa pia na Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dr. James Matargio ambaye alipata fursa ya kuitangaza Tanzania kwa kuonyesha fursa zilizopo katika sekta ya Mafuta na Gesi nchini.
Dr. Mataragio alisema “ pamoja na kuwa bei za mafuta zinaendelea kushuka, bado kuna fursa ya kutumia gesi kusaidia upatikanaji wa nishati endelevu na yenye kulinda mazingira kwa vizazi vya sasa na baadae”
0 comments:
Post a Comment